IQNA

Mtawala wa Myanmar anayewaangamiza Waislamu akwepa kikao cha UN

18:51 - September 12, 2018
Habari ID: 3471668
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi wa Myanmar, Aung San Suu Kyi, amekwepa kuhudhuria kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York wiki ijayo huku akiendelea kulaumiwa kutokana na mauaji ya kimbari ya Waislamu wa jamii ya Rohingya nchini humo.

Suu Kyi, ambaye ni mshindi wa Tuzo ya 'Amani' ya Nobel ni kiongozi wa serikali ya Myanmar na cheo chake ni kansela ambacho ni sawa na waziri mkuu. Aidha yeye pia ni waziri wa mambo ya nje wa Myanmar.

Suu Kyi amepunguza safari zake nje ya nchi kutokana na wito unaotoelwa na taasisi za kimataifa za kutaka watawala wa Myanmar, hasa makamanda wa jeshi, wapandishwe kizimbani kujibu mashtaka kuhusu maangamizi ya umati  ya Waislamu wa jamii ya Rohingya katika jimbo la Rakhine nchini humo.

Wimbi jipya la jinai dhidi ya Waislamu Rarohingya  zilishika kasi tangu tarehe 25 mwezi Agosti mwaka jana. Hadi sasa  jinai hizo zimepelekea kuuliwa Waislamu zaidi ya elfu sita na kujeruhiwa maelfu ya wengine huku wengine karibu laki nane wakilazimika kuwa wakimbizi katika nchi jirani ya Bangladesh.

Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa Zeid Ra'ad Al Hussein amesema kuwa uhalifu unaofanywa na Mabudha kwa himaya ya serikali nchini Myanmar dhidi ya Waislamu wa jamii ya Rohingya ni mauaji ya kimbari.

Al Hussein anasisitiza kwamba, kuna udharura wa kufika katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo na kufanya uchunguzi kuhusu ukatili unaofanywa na serikali ya Myanmar dhidi ya Waislamu.

Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC, imesema inatafakari kuhusu kuanzisha uchunguzi kuhusu ukatili wanaotendewa Waislamu wa jamii ya Rohingya.

3466744

captcha