IQNA

Rais Rouhani: Taifa la Palestina litarejea Quds Tukufu

15:59 - May 05, 2021
Habari ID: 3473880
TEHRAN (IQNA)- , Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameashiria siku ya Kimataifa ya Quds inayoadhimishwa Ijumaa na kusema: "Wiki hii tuna Siku ya Quds. Hii ni siku ambayo ni fakhari kwa mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na ni kati ya wosia wa Imam Khomeini (MA).

Akihutubu katika kikao cha kila wiki cha baraza la mawaziri mjini Tehran, Rais Rouhani ameongeza kuwa: "Taifa la Palestina litarejea katika ardhi zake na mji wa Quds, pamoja na Msikiti wa Al Aqsa, qibla cha kwanza cha Waislamu, vitarejea kwa Waislamu."

Rais Rouhani ameutaja utawala wa Kizayuni wa Israel kuwa adui wa taifa la Palestina na mataifa mengine ya eneo huku akisisitiza kuwa kitendo cha utawala huo kukalia kwa mabavu ardhi za Palestina hakitadumu milele.

Aidha amesema mwaka huu, Siku ya Kimataifa ya Quds itakuwa siku ya maombolezo kwa Wazayuni.

Ikumbukwe kuwa, Imam Khomeini MA Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alitangaza kuwa Ijumaa ya mwisho ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni Siku ya Kimataifa ya Quds. 

Waislamu na wapenda haki wamekuwa wakifanya maandamano katika pembe mbalimbali za dunia kila mwaka katika Siku ya Kimataifa ya Quds, na kubainisha hasira zao kwa siasa za kibaguzi na kikatili zinazotekelezwa na utawala wa Kizayuni dhidi ya wananchi madhulumu wa Palestina.

Mwaka huu Siku ya Kimataifa ya Quds itakuwa Ijumaa Mei 7.

Kwingineko katika hotuba yake, Rais Hassan Rouhani amesema vikwazo dhidi ya nchi hii vimesambaratishwa.

Ameongeza kuwa: "Upande wa pili unafahamu kuwa hauna njia nyingine ghairi ya kurejea katika sheria na ahadi zake katika mapatano ya nyuklia ya JCPOA."

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameendelea kusema kuwa: "Leo ni siku ya maombolezo kwa Wazayuni ambao kupitia Marekani walianzisha vita vya kiuchumi dhidi ya Iran."

Ameongeza kuwa Wazayuni sasa wako katika mkondo wa kusambaratika kikamilifu na pia njama zao za kuibua ufa baina ya Iran na nchi za eneo zimegonga mwamba.

Rais Rouhani amesema njia ya kufika ukingoni vikwazo iko wazi na kwamba haki za taifa la Iran lazima zizingatiwe kikamilifu katika mapatano ya JCPOA. Aidha amesema Iran haitafumbia macho haki zake zote.

3969354

captcha