IQNA

Sayyid Nasrallah: Utawala wa Kizayuni wa Israel unakaribia mwisho wa uhai wake

14:27 - May 07, 2021
Habari ID: 3473885
TEHRAN (IQNA)- Katibu Mkuu wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Hizbullah ya nchini Lebanon amesema utawala wa Kizayuni wa Israel unakaribia mwisho wa uhai wake.

Sayyid Hassan Nasrallah, Katibu Mkuu wa Hizbullah ameyasema hayo katika hotuba iliyorushwa hewani na Televisheni ya Al Manar na kuongeza kuwa: “Uhai wa Israel utafika ukingoni hivi karibuni. Ni machache sana yaliyobakia katika uhai wake.”

Aidha amesema hatua ya baadhi ya nchi za Kiarabu kuanzisha uhusiano na utawala wa Kizayuni wa Israel haitaweza kuulinda utawala huo na kuongeza kuwa hivi sasa utawala wa Kizayuni unakabiliwa na migogoro ya kina ya kisiasa, kijamii na kimaadili.

Sayyid Nasrallah ametoa kauli hiyo kwa mnasaba wa Siku ya Kimataifa ya Quds ambayo inaadhimishwa Ijumaa ya leo.

Kiongozi wa Hizbullah amewapongeza watu wa Palestina kwa kuendeleza mapambano dhidi ya utawala wa Kizayuni huku akisisitiza kuwa, kufungamana Wapalestina na ukombozi wao kutaifanya dunia isisahau kadhia ya Palestina.

Kiongozi wa Hizbullah amesisitiza kuwa harakati za muqawama na mapambano ya Kiislamu zinafungamana na kadhia ya ukombozi wa Palestina. Aidha amewatahadharisha Wazayuni wa Israel kuwa, iwapo hawataondoka Palestina, basi watalazimishwa kurejea walikotoka kwa njia zinginezo. Amesisitiza kuwa, “Palestina ni ya Wapalestina,…na si ya walowezi Waisraeli, maghasibu au wakoloni.”

Aidha amemuenzi kamanda wa zamani wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) Luteni Jenerali Qassem Soleimani kutokana na jitihada zake za kupigania ukombozi wa Palestina. Shahidi Soleimani aliuawa aktika hujuma ya utawala Marekani karibu na uwanja wa ndege wa Baghdad  Januari 2020.

Imam Khomeini MA Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alitangaza kuwa Ijumaa ya mwisho ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni Siku ya Kimataifa ya Quds. 

Waislamu na wapenda haki wamekuwa wakifanya maandamano katika pembe mbalimbali za dunia kila mwaka katika Siku ya Kimataifa ya Quds, na kubainisha hasira zao kwa siasa za kibaguzi na kikatili zinazotekelezwa na utawala wa Kizayuni dhidi ya wananchi madhulumu wa Palestina.

474638

captcha