Kwa mujibu wa maafisa wa Iraq, wafanyaziara sasa wanaendelea kuondoka hatua kwa hatua kutoka Kadhimiya baada ya maombolezo. Kulikuwa Moukeb 2,000 ( Moukeb ni sehemu za kupumzikia zenye suhula na huduma maalum kwa wafanyaziyara) na watoa huduma 5000 wajitolea kuwahudumia wafanyaziayra ambao wengi hufika eneo hilo takatifu kwa miguu kutoka miji ya karibu na ya mbali.
Ikumbukwe kuwa, tarehe 25 Rajab miaka 1261 iliyopita, Imam Musa Kadhim (AS) mmoja wa wajukuu watoharifu wa Mtume Muhammad (saw) aliuawa shahidi. Imam Kadhim (AS) alizaliwa mwaka 128 Hijiria huko katika eneo la Ab'waa lililoko baina ya miji mitakatifu ya Madina na Makka. Mtukufu huyo alipata malezi na elimu kutoka kwa baba yake ambaye ni Imam Ja'far as-Swadiq (as) kwa kipindi cha miaka 20. Baada ya kuuawa baba yake, Imam Kadhim (AS) alipata fursa ya kuongoza Umma wa Kiislamu kwa muda wa miaka 35, na alikumbana na mateso na mashaka mengi katika njia hiyo. Katika zama zake ambazo zilisadifiana na ustawi mkubwa wa utamaduni na elimu ya Kiislamu pamoja na kuimarishwa uhusiano na mataifa ya kigeni, Imam alifanya juhudi kubwa za kueneza mafunzo ya Kiislamu katika mataifa hayo kupitia wanafunzi wake. Mbali na hayo, Imam pia aliendesha mapambano makali dhidi ya watawala dhalimu wa Bani Abbas. Hatimaye Haroun Rashid kutoka ukoo wa Bani Abbas aliyehofia sana kuporomoka kwa utawala wake, alimfunga jela Imam Kadhim (AS). Licha ya kufungwa jela lakini Imam (AS) hakusimamisha shughuli zake za kulingania dini na kupambana na madhalimu. Hatimaye Haroun Rashid alimuua mjukuu huyo wa Mtume (SAW) kwa kumpa sumu.
3482511