Kwa mujibu wa taarifa maelfu ya wananchi wa Iraq kuanzia jioni ya jana Jumapili wamekusanyika kwa wingi kwenye barabara ya uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Baghdad katika sehemu wanajeshi magaidi wa Marekani walipomuua kigaidi Luteni Jenerali Qasem Soleimani, aliyekuwa Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC.
Luteni Jenerali Qassem Soleimani aliuawa shahidi akiwa pamoja na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu wa Mkuu wa Kikosi cha Kujitolea cha Wananchi wa Iraq maarufu kwa jina la Hashd al Shaabi miaka miwili iliyopita wakati rais wa wakati huo wa Marekani, Donald Trump alipotoa amri ya kufanyika jinai hiyo iliyoendeshwa na wanajeshi magaidi wa Marekani kwa kutumia droni yaani ndege isiyo na rubani. Mashujaa hao wawili wa muqawama waliuawa kidhulma wakiwa pamoja na wanamuqawama wenzao wanane.
Mamia ya magari yaliyokuwa yamejaa wapenzi na wafuasi watiifu wa mashujaa hao kutoka maeneo tofauti ya Iraq wameelekea kwenye eneo hilo kushiriki kwenye kumbukumbu hizo.
Mamia ya misafara ya Husaini nayo imeelekea kwa miguu katika eneo hilo kutoka sehemu mbalimbali za Iraq ili kutangaza utiifu wao kwa njia ya mashujaa hao na kuonesha hasira zao kwa wanajeshi magaidi wa Marekani.
Kumbukukmbu za mwaka wa pili wa kuuawa shahidi Luteni Jenerali Qasem Soleimani zinaendelea kwa namna mbalimbali ndani na nje ya Iraq huku Mkuu wa Muungano wa kisiasa wa al Fat-h nchini Iraq, Hadi al A'meri akisisitiza kuwa, Wairaqi wana deni kubwa kwa shahidi Qasem Soleimani na shahidi Abu Mahdi al Muhandis.