Ayatullah Sayyid Ali Khamenei , Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo leo Jumatano mjini Tehran wakati alipokutana na kuzungumza na mkuu pamoja na wajumbe wa duru mpya ya Halmashauri ya Kuainisha Maslahi ya Mfumo wa Kiislamu. Katika kikao hicho amesisitiza kuwa katika matukio ya hivi karibuni nafasi na mchango wa adui umebainika wazi na kuwa dhahiri kwa kila mtu, hata kwa wachambuzi wa nchi ajinabi wasioegemea upande wowote.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa, hivi sasa imebainika wazi kikamilifu kuhusu vitendo vya adui kama vile vya kuendesha propaganda, kufanya kila njia za kuathiri fikra za waliowengi, kuibua hisia mbalimbali miongoni mwa jamii, kufanya uchochezi na hata kutoa mafunzo kuhusu namna ya kutengeneza mada za milipuko na kusababisha moto.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema nukta muhimu katika kadhia hizi, ni hatua na radiamali ya haraka iliyodhihirishwa na adui na kubainisha kuwa taifa la Iran lilitekeleza harakati kubwa katika muda mfupi ambayo ilikuwa digrii 180 mkabala wa sera za mabeberu wa dunia na hivyo maadui kulazimika kuchukua hatua; ambapo katika fremu hiyo waliratibu njama na mipango mbalimbali na kutumia pesa na hivyo kuwaingiza katika maidani watu mbalimbali wakiwemo wanasiasa huko Marekani, barani Ulaya na katika maeneo mengine mbalimbali duniani.
Ayatullah Khamenei amebainisha kuwa harakati hizo adhimu zimeonyesha kwamba mbali na kuwa taifa la Iran ni taifa lenye uchangamfu, ustaarabu, kushikamana na thamani za kidini pia ni taifa linaloendelea mbele kwa kasi kubwa ya maendeleo.
Wakati huo huo, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekutaja kushiriki mamilioni ya vijana katika matembezi ya arubaini na harakati za kiimani kuwa ni mfano wa ucha-Mungu na harakati kubwa za taifa la Iran na kuongeza kuwa, kwa hakika ubunifu umekuwa mikononi mwa taifa la Iran na kumpelekea adui alilazimike kutoa jibu la kipumbavu, la pupa na kuratibu mipango yake kwa ajili ya kuibua ghasia.
4091328